Pages

Monday 12 January 2015

Gari la DC wa Mbozi lazua tafrani jimboni kwa Kilango

Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela  akizozana na  dereva wa mkuu wa wilaya ya Mbozi (aliyekataa kutaja jina lake) baada ya kukuta gari la mkuu huyo wa wilaya likipeperusha bendera katika jimbo la Same Mashariki jambo ambalo ni kinyume cha taratibu.Picha na Rehema Matowo 

Same. Katika hali isiyo ya kawaida, Mkuu wa Wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya, Dk Michael Kadege limekutwa likipeperusha bendera katika eneo la Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro na kuzua tafrani kati ya mkuu huyo na Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela.
Gari hilo likiwa na Bendera ya Taifa, lilionekana saa nne asubuhi likiwa limeegeshwa katika eneo la Mamba Myamba katika Jimbo la Same Mashariki huku Dk Kadege akiwa kwenye mgahawa.
Kitendo cha gari hilo kuonekana likipeperusha bendera kilimfanya Kilango kulifuata akidhani ni la Mkuu wa Wilaya ya Same, ndipo akakuta ni la Mbozi.
“Hili gari siyo la Same na kawaida mkuu wa wilaya nyingine haruhusiwi kupeperusha bendera kwenye eneo ambalo siyo lake, huyu amekuja kwenye mambo yake ya siasa, anapeperusha bendera ili wananchi wamwone kuwa yuko juu na hii ni hujuma kwenye jimbo langu,” alilalamika Kilango.
Alisema Dk Kadege ni miongoni mwa watu wanaotaka kugombea ubunge Jimbo la Same Mashariki lakini ni vyema akasubiri muda ukifika ajitokeze hadharani badala ya kujenga mpasuko kwa CCM katika jimbo hilo.
“Huyu amekuja kwa ajili ya vikao vya ndani, mwaka 2005 tuligombea wote kwenye kura za maoni nikamshinda nikiwa na kura 389 yeye 46 akawa mtu wa nne, mwaka 2010 mimi nilipata kura 7,900 na yeye alipata 2,200 sasa ameanza, sikatai lakini asubiri muda wake,” alisema Kilango.
Kwa upande wake, Dk Kadege alisema hakuwa na taarifa kuwa gari lake linapeperusha bendera kwa kuwa yeye hahusiki kuweka bendera, akataka dereva wake aeleze sababu za kupeperusha bendera kwenye eneo lisiloruhusiwa.
Dk Kadege alisema yeye yuko likizo na alikwenda nyumbani kwao Same kupumzika na hafanyi shughuli zozote za kisiasa katika jimbo hilo kama inavyodaiwa na Kilango.
Dereva wa mkuu huyo wa wilaya ambaye alikataa kutaja jina lake, alipohojiwa sababu za kupeperusha bendera katika eneo lisiloruhusiwa alisema alikuwa akifanya usafi wa gari na alipohojiwa zaidi alidai siyo msemaji wa mkuu wa wilaya.
Mkuu wa Wilaya ya Same, Herman Kapufi alisema kutokana na sheria, utaratibu na miongozo ya wakuu wa wilaya, kiongozi huyo wa wilaya haruhusiwi kupeperusha bendera katika eneo ambalo siyo lake.
Alisema kwa mujibu wa Sheria ya Tawala za Mikoa namba 19 ya Mwaka 1997 na Sheria ya Serikali za Mitaa namba Saba na Nane ya mwaka 1982, mkuu wa wilaya ni msimamizi wa shughuli za kimaendeleo na mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama katika wilaya yake tu.
Kapufi alisema atawasiliana na Dk Kadege kama anafahamu utaratibu na miongozo waliyopewa wakati wa kuanza kazi ili ajue kama alikusudia kufanya hivyo au kama alipitiwa.

Chanzo Gazeti la Mwananchi

No comments: